Saturday, August 23, 2014

HONGERA BEN SAANANE

Maamuzi Rasmi juu ya barua yangu ya mgogoro wa kikanuni/masharti ya uchaguzi wa baraza la vijana Chadema(BAVICHA) Taifa yamefanyika.
Fomu za uchaguzi zilizotolewa tarehe 12/08/2014 , liliwekwa sharti kuwa mgombea awe na miaka 18-30(Awe amezaliwa 1984 na kuendelea).
Sharti hili lililowekwa kwenye mabano lilinisukuma ku-challenge kanuni/masharti/mahesabu hayo pamoja na masharti mengine kwa kufuata taratibu za chama kama nilivyowaeleza na nikaahidi kusubiri uamuzi
Hoja yangu ilikua kama aliyezaliwa tarehe 01.01.1984 ana haki ya kugombea kwanini isiwe mimi niliyezaliwa tarehe 13/12/1983 yaani wiki mbili na nusu kabla yake kwa kuwa hadi siku ya uchaguzi atakua na miaka 30 na miezi 9 na siku 10 wakati mimi nitakua na miaka 30 na miezi 9 na siku 28 halikadhalika yule aliyezaliwa tarehe 11/09/1983 atakua na miaka 30 na miezi 11 na siku 30 hadi siku ya uchaguzi tarehe 10.09.2014.
Na kwamba ingekua sahihi kama sharti hilo "SHARTI NDANI YA MABANO" lingetamka sawi kuwa mgombea asiwe amefikisha miaka zaidi hadi ifikapo siku ya uchaguzi.Hii ndio ilikua hoja yangu.
Nilirejea katiba na miongozo yetu na kanuni za uchaguzi uliopita wa Baraza la Vijana uliofanyika Mwezi Mei 2011.
Maamuzi ni kuwa wagombea waliozaliwa kuanzia mwaka 1984 ndio watakaokuwa eligible kugombea kama inavyoonekana kwenye fomu zitakazojazwa na wagombea na zipo pia kwenye tovuti ya chama.
Kutokana na maamuzi haya nasikitika kuwatangazia vijana wenzangu kuwa ,kufuatia "SHARTI HILO NDANI YA MABANO " NIMEJIENGUA RASMI KATIKA KINYANG'ANYIRO CHA UCHAGUZI KUWANIA NAFASI YA JUU KUONGOZA BARAZA LA VIJANA CHADEMA (BAVICHA).
Maandalizi mliyonishauri niendelee nayo wakati nasubiri uamuzi yatasitishwa
Maandalizi yote ya mkutano na waandishi wa habari kesho Travertine Hotel tumeyasitisha rasmi,Maandalizi ya kurejesha fomu jumatatu ambayo jeshi la polisi liliarifiwa na kukiri kupokea barua iliyoandikwa na vijana waliotaka kunisindikiza kurejesha fomu kuanzia viwanja vya BIAFRA kuelekea Makao makuu yamesitishwa.
Kwa moyo wa kipekee na kwa unyenyekevu mkubwa,nawashukuru marafiki zangu wa karibu na wa mbali,nawashukuru marafiki wa BAVICHA kwa maandalizi kabambe ya kampeni,Nawashukuru ninyi marafiki zangu hapa Facebook na mitandao mingine kwa kuniunga mkono kwa wingi wenu na kujitolea kupambana na dhuluma na hila chafu chafu za watu wachache sana waliokua wakifanya siasa chafu katika safari hii.Mlijitolea kulinda haki,misingi na falsafa ya chama chetu na pia principle zenu kwa kile mnachoamini bila woga.Mlisimama kidete
Ninyi mmekua Nanga yangu initulizayo katika dhoruba.
Ninatambua thamani na mchango wenu kwangu.
Kuna wale walioomba kuchangia kampeni na ziara yangu,ziara ya kufufua ndoto ya mashujaa wetu na kuitaka/kuirudisha Tanzania (Reclaiming Tanzania ).
Sina cha kuwalipa. Nawashukuru sana kwa kusimama nami . Mwenyezi Mungu awajalie kila lililo la kheri nanyi.
Ninafarijika na kuona fahari kuwa chama chetu kimekua sambamba na kasi ya ukuaji wa Teknolojia pengine kuliko chama kingine nchini.
Haikushangaza sana kuona idadi kubwa ya viongozi waliochaguliwa kwenye majimbo na wilaya na hasa tuko nao hapa na kwenye mitandao mingine kama Watsap.
Hakika kampeni za uchaguzi huu tungefanya mageuzi makubwa ya matumizi ya mitandao katika siasa.
Wale wote waliong'ang'ania fikra za ukale(Primitive mentality) tungewaziba midomo.
Mara kadhaa kupitia mitandao hii na ana kwa ana nimekua nikihimiza wale wote wenye nia na dhamira ya kupigania mabadiliko wajitokeze kwa wingi kugombea nafasi za uongozi.
Wengi walifanya hivyo na walishinda kwa kishindo na hata chaguzi za mikoa.
Chama chetu kimekua kuliko wakati mwingine wowote.
Chama ni kikubwa kuliko sisi.Tukilinde kama mboni ya jicho .
Kukilinda CHADEMA hata kujitoa sadaka binafsi,ni Sadaka kwa Mageuzi na sadaka hii ni hazina isiyooza kwa vizazi vijavyo vya watanzania.
Mwenyezi Mungu atulinde.
Tusikubali kuingia katika majaribu au mitego yoyote itakayotugawa.Tusikubali kuwa katika upande mbaya wa historia ya harakati za mageuzi.
Safari bado ni mbichi,tutizame tulikotoka na kisha tutazame mbele.Wapo waliofukuzwa /kunyimwa kazi (Mimi ni mmojawapo) ,walioachwa ,waliojeruhiwa na kupata ulemavu na waliopoteza maisha kwa ajili ya CHADEMA na kutafuta haki za kiraia.
Tuendelee kujiimarisha kama taasisi na ni rai yangu kuwa ukomavu wa kisiasa unahitajika zaidi kutokana na ukweli kuwa uchaguzi ndani ya chama ni mgumu kuliko unapopambana na wagombea kutoka nje ya chama.
Ni katika uchaguzi kama huu ,marafiki na mahasimu watajipambanua lakini kitu bora na cha muhimu zaidi mahasimu wanapoonyesha uhasimu katika hoja huwaimarisha wote pamoja na taasisi tofauti na wale wenye siasa za mitaroni.Hao ni kuwapuuza na kusonga mbele.
Tuendelee kuogelea kuelekea kina kirefu zaidi.
Wale wenye hila na nia ovu kama mlivyoshuhudia siku za karibuni,wasisahau kuwa tutaendelea kukutana kwenye kordo za siasa.I'm there to stay.
Sitawafuata kwenye huko vichochoroni kwenye mitaro ya "SIASA MAJITAKA".
Historia kwangu sio gereza,bali ni darasa.Kuna wale waliowahi(labda Walitabiri) na kuandika kwenye mitandao ya kijamii hata kabla fomu hazijatolewa kuwa Mwisho wa Ben Saanane Umefika.Wajitafakari Upya.
Uamuzi huu Sio alama ya Nukta,Bali ni alama ya Mkato Katika Safari yangu ya Kisiasa.Wala sio alama ya Mabano.
Nilipoenguliwa uchaguzi wa BAVICHA mwaka 2011 kwa tuhuma za kuunda Alliance haikua alama ya Nukta katika Safari Yangu.
Nilipoadhibiwa na Baraza la Vijana ambapo mojawapo ya makosa ilikua kutoa tuhuma za usaliti hadharani dhidi ya aliyekuwa naibu katibu Mkuu Zitto Kabwe Tarehe 5 January 2013 na kuzuiwa kugombea nafasi yoyote ndani ya baraza la vijana kwa muda wa mwaka 1 haikua alama ya nukta, bali ilikua alama ya mkato katika safari yangu kisiasa.
Kama nilivyowaahidi ,nitaendelea kukilinda na kukijenga chama chetu na safari hii ya mapambano imezidi kutiwa chachu.
Kuna kisa kimoja cha kifalsafa kwenye Biblia.Kisa cha Mama aliyeiba Mtoto na kesi kupelekwa kwa mfalme Sulemani baada ya utata mkubwa juu ya mams halisi wa mtoto na baina ya wanawake wawili waliokua wanamgombania.Aliamuru Panga liletwe mbele yake kisha mtoto akatwe ili wagawane sawa.Mwanamke Mmojawapo akaridhia haraka wakati mwingine alijibu 'Ewe Mfalme,Ni bora akabidhiwe huyu mwenzangu ' Busara zikamtuma Sulemani kuwa Mama halisi ni yule mwenye uchungu na mtoto.Tusiruhusu sasa kuingia upande mbovu.
Nimepokea Ushauri mwingi kutoka kwa ndugu,jamaa na marafiki .Msiumie kwa uamuzi huu,tuuheshimu .
Tutaendelea kuwaabisha wale wote wa nje wanaotazama uchaguzi wetu wa ndani kwa jicho la husuda.Maadui wa demokrasia na haki tutawashinda kwa ukomavu wetu wa kisiasa tu.
Kaka yangu Godbless Lema na baadhi ya wabunge vijana na madiwani wetu, nimeheshimu Ushauri wenu.Dada yangu Halima Mdee nimeendelea na nitaendelea kuheshimu ushauri wako.
Nina maamuzi mengine nitakayochukua baada ya kutafakari kwa kina ndani ya saa 48 zijazo.
Mwanamapinduzi Ninayemuhusudu sana Rais wa Zamani wa Venezuela Hugo Chavez alishawishi na ameendelea kunichochea kwa kauli yake kwenye nukuu siku siku zote "There is no turning Back".
Mwenyezi Mungu awabariki nyote.
Aluta Continua ,Victory Ascerta....


CHANZO MTANDAO WA WANABIDII.

No comments:

Post a Comment